Thursday, March 21, 2013

WAFUASI 52 WA SHEIKH PONDA WAFUNGWA JELA MWAKA MMOJA.

Wafuasi wa Ponda wakipanda kalandinga kwenda jela baada ya kuhukumiwa jela  mwaka mmoja 
WAKATI kesi inayomkabili Katibu wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Ponda Issa Ponda, ikiendelea katika Mahakama ya hakimu Mkazi Kisutu wafuasi wake 52 kati ya 53 waliokuwa wakikabiliwa na kesi ya maandamano haramu wamehukumiwa adhabu ya kifungo cha mwaka mmoja jela.

Hata hivyo mahakama hiyo ilimwachia huru mshtakiwa mmoja, Waziri Omar Toy, ambaye alikuwa mshtakiwa wa 48 katika kesi hiyo baada ya kuridhika
kuwa hana hatia kutokana upande wa mshtaka kushindwa kuthitibisha mashtaka dhidi yake.

Wafuasi hao wa Ponda walihukumiwa adhabu hiyo na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya kupatikiana na hatia katika makosa matatu yaliyokuwa yakiwakabili kati ya manne.

Wafuasi hao wa Ponda walikamatwa Februari 15 wakidaiwa kufanya maandamano haramu kwenda kwa Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) kwa lengo la kumshinikiza aondoe zuio la dhamana dhidi ya Ponda na mwenzake, Mukadamu Swalehe, wanaokabiliwa na kesi ya uvamizi wa kiwanja cha Chang’ombe Markazi.


Akisoma hukumu hiyo Hakimu Mkazi Sundi Fimbo alisema kuwa baada ya kusikiliza ushahidi na hoja za pande zote pamoja na vielelezo vilivyowasilishwa mahakamani hapo ameridhika, kuwa upande wa mashtaka umeweza kuthibitisha mashtaka matatu dhidi ya washtakiwa hao.
“Katika kosa la kwanza ninawahukumu kifungo cha mwaka mmoja jela, na kosa la pili pia mwaka mmoja jela na tatu mwaka mmoja jela. Adhabu zote
zinakwenda kwa pamoja.”alisema Hakimu Fimbo.

Aliyataja mashtaka hayo ambayo washtakiwa walipatikana na hatia kuwa ni shtaka la kwanza la kula njama za kutenda makosa, la pili, kufanya maandamano yaliyozuiwa na Jeshi la Polisi na la tatu kufanya mikusanyiko haramu na kusababisha uvunjifu wa amani.

Hata hivyo Hakimu Fimbo alisema kuwa katika shtaka la nne la uchochezi wa kutenda kosa lililokuwa likiwakabili washtakiwa wanne, upande wa mashtaka umeshindwa kulithibitisha.
“Mahakama imeridhika na ushahidi uliwasilishwa na upande wa mashtaka kuwa umethibitisha mashtaka dhidi ya washtakiwa wote isipokuwa mshtakiwa wa 48.”, alisema Hakimu Fimbo na kuongeza: “Hivyo mahakama imewatia hatiani washtakiwa wote isipokuwa mshtakiwa wa 48, katika shtaka la kwanza, la pili na la tatu, na katika shtaka la nne, mahakama imeona kuwa washtakiwa hawana hatia.”

No comments:

Post a Comment