Saturday, September 14, 2013

PADRI AMWAGIWA TINDIKALI ZANZIBAR


 

Padri wa Kanisa la Romani Katoliki Parokia ya Machui, Joseph Monesmo Magamba amemwagiwa tindikali na watu wasiojulikana katika Mtaa wa Mlandege jana jioni, Mkoa wa Mjini Magharibi, Zanzibar.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Haji Hana alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba kiongozi huyo wa dini amelazwa katika Hospitali ya Mnazi Mmoja, akiendelea na matibabu baada ya kujeruhiwa usoni, kifuani na mikononi.
Hana alisema kwamba Padri Magamba (60) alikuwa akitokea katika duka la huduma za mawasiliano ya mtandao la Shine Shine saa 10.15 jioni na watu waliommwagia walimtega mlangoni kabla ya kufanya uhalifu huo na kutoweka kwenye vichochoro vya Mitaa ya Mtendeni na Mchangani.
Alisema polisi wamestushwa na tukio hilo kwa vile limetanguliwa na matukio matatu ya kumwagiwa tindikali kwa viongozi wa dini na kuwataka wananchi kutoa ushirikiano wa kufanikisha kuwakamata watu wanaojihusisha na vitendo hivyo.
Hili ni tukio la tano kutokea visiwani Zanzibar ambapo Septemba 13 mwaka huu, Sheha wa Shehia ya Tomondo, Wilaya ya Magharibi Unguja, Mohammed Omar Said (65), alimwagiwa tindikali na mtu asiyejulikana wakati alipokuwa akichota maji nje ya nyumba yake.

Desemba mwaka jana, padri Ambrose Mkenda wa Kanisa Katoliki Zanzibar alipigwa risasi na Februari 17 mwaka huu, padri Evarist Mushi wa kanisa hilo aliuawa kwa kupigwa risasi wakati akienda kuongoza ibada ya Jumapili katika Kanisa la Mtakatifu Teresia.

Novemba 5, 2012, Katibu wa Mufti wa Zanzibar, Sheikh Fadhil Soraga, naye alimwagiwa tindikali na watu wasiojulikana wakati akifanya mazoezi katika kiwanja cha Mwanakwerekwe.
Agosti 7 mwaka huu raia wawili wa Uingereza walimwagiwa tindikali kwenye eneo la Mji Mkongwe visiwani Zanzibar "Stone Town".

Wasichana hao wawili wa miaka 18 walikuwa walimu wa kujitolea katika shule moja ya Kanisa la Anglikana visiwani humo.

CHANZO: MWNANCHI/ T. DAIMA

No comments:

Post a Comment