Wednesday, January 22, 2014

UFAFANUZI KUHUSU UPANUZI NA MGOGORO KUHUSU UPANA WA BARABARA YA MOROGORO

Mosi, Serikali kutoa ahadi bila utekelezaji kwa miaka mingi. Mwaka 2012 na 2013 Waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli amekuwa akirudia kauli kwamba ujenzi wa Dar Es Salaam-Chalinze express road kuanza. Katika mkutano wangu na wananchi jimboni tarehe 19 Januari 2014 kuhusu ujenzi wa Barabara hiyo, nimesisitiza kwamba fedha za ujenzi wa barabara hiyo hazijatengwa hivyo ujenzi hauwezi kuanza. Badala yake nilifafanua kwamba Serikali inachokifanya kwa sasa ni kutafuta mkandarasi mwenye uwezo wa kutafuta fedha na kujenga. Hivyo, ni muhimu Serikali ikawaeleza wananchi ukweli na kuharakisha kutekeleza ahadi zilizotolewa kwa miaka mingi.

Pili; badala ya Serikali kuja na wazo la kujenga njia zaidi ya 6, ianze kwanza kutekeleza ahadi ya njia hizo sita; kwa kuanza na ujenzi katika umbali wa mita 60 zilizopo. Hivyo, sioni haja ya Serikali kujenga kwa sasa mpaka eneo la upana wa mita 241 wakati ambapo kuna barabara nyingine muhimu za pembezoni ya Barabara ya Morogoro ambazo zikiharakishwa kujengwa zinaweza kupunguza foleni mf. Barabara ya Goba-Mbezi-Msigani-Malambamawili-Kinyerezi na nyinginezo ambazo ujenzi wake unasuasua.